Dk Shein aliyasema hayo jana, Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi Mteule wa Tanzania nchini Burundi, Rajab Hassan Gamaha ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya kuaga na kupata baraka za rais.
Katika mazungumzo hayo, Dk Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua juhudi kubwa za kuiimarisha sekta ya utalii hapa nchini sambamba na kuimarisha vivutio vyake kwa wageni kutoka nchi mbalimbali duniani zikiwemo nchi za Maziwa Makuu kama vile Burundi.
Dk Shein alieleza kuwa ni imani yake kubwa kuwa migogoro iliyopo nchini humo hivi sasa itamalizika kwa msaada mkubwa wa viongozi wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao wamekuwa wakichukua juhudi za makusudi za kuhakikisha migogoro iliyopo nchini humo inamalizika.
Alisema kuteuliwa kwa Balozi huyo kuiwakilisha Tanzania nchini humo ni hatua mojawapo ya Tanzania kuendelea kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kidugu, kidamu na kimipaka na Burundi.
Dk Shein alisema hivi sasa wananchi walio wengi wa Burundi wameanza kujifunza lugha ya Kiswahili na Zanzibar ni sehemu yenye asili ya lugha hiyo, hivyo ipo haja ya kuwahamasisha wananchi wa Burundi kuja Zanzibar kujifunza lugha hiyo kwenye Chuo chake Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).
Aidha, Dk Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi Gamaha kuwa wakati ukifika Zanzibar itafanya uchaguzi wake ulio huru na haki huku akieleza matumaini yake kuwa viongozi wa vyama vya siasa watafuata matakwa ya Serikali katika kusimamia amani na utulivu.
No comments:
Post a Comment