Profesa Muhongo apinga Tanesco kununua transfoma kampuni binafsi


Waziri wa Nishati ya Madini, Profesa Sospeter Muhongo amepinga uamuzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), kutumia zaidi ya Sh15 milioni kununua transfoma katika kampuni binafsi badala ya kwenye Kiwanda cha Tanalec Limited ambacho shirika hilo lina hisa zake.

Profesa Muhongo alitoa uamuzi huo baada ya kutembelea kiwanda hicho jana akiongozana na maofisa wa Tanesco, Wakala wa Umeme Vijijini (Rea) na maofisa wa wizara hiyo.

Katika ziara hiyo walibaini kuwa Tanesco hainunui transfoma katika kiwanda hicho.

“Kuacha kununua Transfoma Tanalec hakuna sababu nyingine zaidi ya rushwa na siyo kweli kuwa Sheria ya Manunuzi inawabana. Kama kweli inawazuia, suala hili nitalifikisha kwa Rais (John Magufuli) na katika ngazi nyingine za uamuzi,” alisema Profesa Muhongo.

Katika kiwanda hicho, Tanesco inamiliki asilimia 20 ya hisa, Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) asilimia 10 na Kampuni ya Transcentury ya Kenya inamiliki asilimia 70.

Awali, kabla ya ubinafishaji Serikali ilikuwa ikimiliki asilimia 80 za hisa.

Kaimu Meneja Mwandamizi wa Manunuzi wa Tanesco, Jasson Katule alisema shirika hilo linashindwa kununua transfoma Tanalec kutokana na sheria kuwabana kwa kuwa inawalazimisha kutangaza zabuni.

Alisema katika zabuni, Tanalec ilishindwa na kampuni za Quality Group na Intertrade ya India.

Kampuni ya Quality Group itanunua transfoma za zaidi ya Dola 3 milioni za Marekani na Intertrade imeshinda zabuni ya Dola5 milioni za Marekani.

Awali, Meneja Mkuu wa Tanalec, Zahir Saleh alisema kiwanda hicho kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha transfoma 10,000, lakini kinazalisha 7,000 kutokana na udogo wake.

Pia, alisema wanakabiliwa na changamoto za kukosa soko la ndani huku wateja wakubwa yakiwa ni mashirika ya umeme ya Kenya, Uganda na Zambia.

Kikwete akubali kuwa balozi wa chanjo Afrika

RAIS mstaafu Jakaya Kikwete amekubali uteuzi wa kuwa Balozi wa Heshima wa kuhamasisha masuala ya afya na kuwataka Wakuu wa Nchi za Afrika kuweka kipaumbele katika upatikanaji wa huduma za afya katika jamii.


Kikwete aliyasema hayo mjini Addis Ababa nchini Ethiopia juzi, wakati akitoa salamu zake baada ya kukubali kuwa Balozi wa Heshima wa ‘Africa United’ kupitia Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na Gavi.

United Africa ni mpango uliobuniwa kusaidia uhamasishaji wa masuala ya afya ukiongozwa na Gavi, CAF, Umoja wa Afrika, Benki ya Dunia na CDC Foundation na wameamua kutumia michezo kama nyenzo mojawapo ya kufanya kampeni ya kuhamasisha jamii juu ya umuhimu wa masuala ya afya yanayolikabili bara la Afrika.

Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti Mwenza wa Jopo la watu mashuhuri la kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa juu ya namna bora ya kuendeleza na kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu hususani katika afya ya uzazi ya mama na mtoto, alisema upatikanaji wa chanjo utasaidia kuokoa vifo vingi vya watoto Afrika.

Uteuzi huo umekuja huku Rais huyo mstaafu akiteuliwa pia kuwa Mjumbe Maalumu wa AU nchini Libya.

Dr. Bana: CCM Iheshimu Mfumo wa vyama Vingi

Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu Cha Dar es salaam ambaye pia ni mchambuzi wa masuala ya kisiasa na mambo ya kijamii Dk Benson Bana amesema chama tawala nchini CCM lazima kikubali utamaduni na kanuni za kukubali mfumo wa vingi vya siasa.


Ameyasema hayo alipokuwa akizungumzia suala la upatikanaji wa Meya wa jiji la Dar es salaam ambapo limegubikwa na mambo ya siasa zizizofaa kwa maendeleo ya wananchi na wapenda demokrasia nchini.

''Kauli za mvutano na malumbano ya UKAWA na chama cha mapinduzi havitasaidia wananchi kwanza wanajidhalilisha, kinachotakiwa ni upinzani kutumia busara lakini chama tawala pia watambue kwamba walipokubali mfumo wa vyama vingi lazima wakubali mabadiliko na kuheshimu mfumo wa vyama vingi

"Hakuna sababu ya msingi ya kuwepo malumbano hadi watu wengine wapigwe na wengine kuwekwa rumande kwanza kazi kubwa ya umeya ni kuongoza vikao ingelikuwa tunatafuta mkurugenzi hapo sawa lakini hili wanakosea kwa kweli''-Amesema Dkt. Bana

Meya wa jiji la Dar es salaam ameshindwa kuchaguliwa mara kadhaa pamoja na kuwepo kwa uhalali wa kufanyika uchaguzi huo jambo ambalo limesababisha malumbano makali na kushikiliwa kwa wabunge wawili wa Chadema Saed Kubenea na Halima Mdee.
==

CHADEMA Kususia ziara na Vikao vya Maendeleo Dar es Salaam


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesusia ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika manispaa za Temeke, Kinondoni na Ilala na kuthibitisha kutoshiriki katika kikao cha bodi ya barabara kinachotarajiwa kufanyika leo kwa kile wanachodai kushinikiza kuachiwa kwa madiwani na mbunge ambao wanaeshikiliwa na jeshi la polisi.

Akielezsea hatua hiyo jana, Meya wa Manispaa ya Kinondoni Boniface Jacob alisema kuwa hawaoni sababu ya kuendelea na vikao mbalimbali vya jiji wakati hawajui hatma ya wenzao ambao mpaka sasa wanashikiliwa na polisi na wengine wanaitwa kufika kituoni hapo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni kusababisha fujo katika zoezi la uchaguzi wa meya wa Jiji la Dar es Salaam.

Kikao kikubwa cha kujadili mipango ya maendeleo ya jiji la Dar es Salaam kinatarajiwa kufanyika leo  ambapo mada kuu itakuwa ni ujenzi wa barabara katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Polisi Wafanya Upekuzi Nyumbani Kwa Halima Mdee


Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam jana lilifanya upekuzi mkubwa katika nyumba ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) baada ya kumtilia shaka kuwa na nyaraka muhimu za vikao vya uchaguzi wa Meya wa Jiji hilo.
Kikosi cha jeshi hilo kilifika katika nyumba ya mbunge huyo majira ya saa tisa alasiri na kufanya mazungumzo na Mwanasheria wake, John Mallya ambapo baada ya kukamilisha taratibu za kisheria walianza zoezi la upekuzi uliochukua zaidi ya saa moja.
Kiongozi wa kikosi hicho cha Polisi, aliwaambia waandishi wa habari kuwa walilazimika kufanya upekuzi katika nyumba hiyo baada ya kusadikika kuwa wakati wa vurugu zilizotokea katika ukumbi wa Karimjee jijini humo wikendi iliyopita kufuatia kuahirishwa kwa uchaguzi wa Meya wa Jiji, Mdee aliondoka na faili muhimu lenye madokezo yanayohusu uchaguzi huo.

Hata hivyo, baada ya kukamilisha upekuzi huo, Polisi walijiridhisha kuwa hakukuwa na nyaraka hizo ndani ya nyumba hiyo wala kitu chochote ambacho wangekitilia shaka licha ya kukuta nyaraka nyingi za mbunge huyo. Hivyo, walitoa cheti maalum cha kuthibitisha kuwa hakuwa na nyaraka zozote kinyume cha sheria.
“Wamekagua nyaraka zote. Madai yao ni kuwa Halima alimpora au alichukua nyaraka za kiongozi wa Jiji, lakini wamekuta hakuna jambo lolote ambalo linatiliwa shaka. Na wametoa Certificate inayoonesha kwamba hakuna chochote ambacho kimechukuliwa,” alisema Mwanasheria wa Mbunge huyo, John Mallya.

Mdee alishikiliwa na Polisi na kulala rumande juzi kutokana na tuhuma za kushiriki katika vurugu zilizotokea katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam, Jumamosi, Februari 27.
Wengine wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi ni Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea na Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara.

Wauguzi sita Temeke wasimamishwa Kazi kwa kuuza gloves


Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamis Kigwangalla amewasimamishwa kazi wauguzi sita katika hospitali  ya  Temeke kwa kosa la kuomba rushwa.
Wauguzi waliosimamishwa ni Hadija Salum, Beatrice Temba, Agnes Mwampashe, Elizabeth Mwilawa, Mariam Mohamed na Marion Said, ambao walikuwa zamu katika wodi ya wajawazito wakati wa tukio hilo.

“Nimewasimamisha kazi wauguzi wote waliokuwa zamu jana (juzi) asubuhi, nakuagiza Msajili wa Baraza la Wauguzi uwasimamishe hadi utakapowasafisha kupitia kamati ya msajili,” alisema Dk Kigwangalla.
Mmoja wa wajawazito, Loshan Seif alisema alipowasili juzi asubuhi kwa ajili ya kujifungua, muuguzi mmoja wa zamu alimtaka kulipia Sh5,000 za gloves.
“Siku zote huwa natumia bima lakini jana (juzi) wakaniambia hawatumii, nitoe Sh5,000 za gloves, baadaye niliambiwa natakiwa kuwa na uzi wa mshono, sindano na vingine hivyo kama sina nitoe fedha,” Seif.
Dk Kigwangalla alifanya ziara ya ghafla hospitalini hapo jana saa 9.00 alasiri.

Akizungumza jana alasiri baada ya kufanya ziara ya ghafla Hospitalini hapo na kupata malalamiko hayo kutoka kwa wanawake waliojifungua.
“Mama anaambiwa atoe fedha ya gloves Sh5,000 wakati dukani zinauzwa Sh1,000, nataka liwe fundisho kwa wote wanaotuongezea vifo vya wajawazito kwa tamaa ndogondogo,” alisema Kigwangalla.
Katika ziara hiyo, Dk Kigwangalla alishuhudia ubovu wa vyumba viwili vya upasuaji na kutoa maelekezo kwamba, virekebishwe ndani ya miezi sita.
“Hali ni mbaya ndani ya hizi ‘theater’ zote mbili zifanyiwe ukarabati iwapo itashindikana nitazifunga, lazima ziwe na hadhi yake na nitakuja kukagua,” alisema.
©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved