Ligi Kuu yaingia patamu

KIVUMBI cha Ligi Kuu Tanzania Bara, kinaendelea tena leo kwenye viwanja vitano tofauti, huku miamba ya soka Yanga na Simba ikirejea tena kusaka pointi tatu. Yanga ambayo kabla ya mechi ya Jumatano iliyotoka sare ya mabao 2-2 na Mwadui FC Uwanja wa Kambarage Shinyanga ilikuwa na pointi 19 sawa na Azam FC ikiongoza ligi hiyo, ilijikuta ikipata matokeo hayo ambayo yaliwapa majonzi mashabiki wao.
Majonzi hayo yaliongezeka zaidi Alhamisi baada ya Azam kuibuka na ushindi wa mabao 4-2 dhidi ya JKT Ruvu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, hivyo Azam kuipiku Yanga kileleni mwa msimamo ikiwa na pointi 22 ikiiacha Yanga nafasi ya pili na pointi zake 20.
Kutokana na hali hiyo, leo Yanga itashuka Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi Tabora kuivaa Kagera Sugar, ikiwa na dhamira moja ya kurejea kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo. Kama Yanga ikishinda leo itafikisha pointi 23 na itaombea Azam FC ambayo kesho itacheza na Toto Africans Uwanja wa Azam Chamazi ipate matokeo mabovu.
Yanga inapewa nafasi ya kushinda leo kutokana na mwenendo mbaya wa wenyeji wao Kagera Sugar, ambao tangu kuanza msimu huu wameshinda mchezo mmoja na kupoteza mitano kati ya tisa waliyocheza.
Leo utakuwa mtihani wa pili kwa Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Mohammed Adolf Rishard, tangu akabidhiwe timu akirithi mikoba ya Mbwana Makatta aliyeachia ngazi kutokana na matokeo mabaya. Ni wazi Kocha Mkuu wa Yanga, Hans Pluijm naye ataingia uwanjani kuhakikisha vijana wake wanaibuka na ushindi ili kuwapa furaha mashabiki wao.
Hata hivyo pamoja na mwanzo mbaya wa Kagera Sugar, lakini timu hiyo inaweza kuzinduka na kufanya maajabu kwa kuifunga Yanga, kwani inakikosi bora cha wachezaji waliodumu kwa muda mrefu na timu hiyo akiwemo nahodha wake George Kavila na Paul Ngwai.
Yanga itaingia kwenye mchezo huo ikizidi kujivunia safu yake ya ushambuliaji inayoongozwa na Mzimbabwe, Donald Ngoma mwenye mabao saba na Amissi Tambwe ambao wamekuwa wakipambana kuhakikisha timu yao inafanya vizuri kwa kufunga mabao mengi.
Kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam, Simba inawakaribisha Majimaji ya Songea huku kocha wake Dylan Kerr, akijivunia ushindi wa bao 1-0, walioupata kwenye mchezo uliopita dhidi ya Coastal Union ya Tanga na timu hiyo kufikisha pointi 18 na kupanda hadi nafasi ya nne.
Mshambuliaji Hamisi Kiiza amekuwa tegemeo kwa kocha Kerr, katika upande wa mabao baada ya kufunga bao lake la sita Jumatano iliyopita ukiwa ni mchezo wake wa kwanza tangu kurejea uwanjani baada ya kukosa mechi tatu kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya nyama za paja.
Pamoja na kuonesha kiwango cha chini kwenye mchezo uliopita, lakini Simba wanapewa nafasi ya kushinda mchezo wa leo kutokana na udhaifu wa wapinzani wao Majimaji waliopo nafasi ya 10 wakiwa na pointi 11.
Rekodi zinaonesha Majimaji imekuwa hatari msimu huu inapocheza nyumbani uwanja wa Majimaji Songea, lakini mambo huwa tofauti inapokuwa ugenini na takwimu zinaonesha imepoteza mchezo mmoja nyumbani na kushinda mitatu, huku ikifungwa michezo mitatu na miwili ikitoka sare.
Mechi nyingine za leo, Mtibwa Sugar inayoshika nafasi ya tatu kwenye msimamo, itakuwa nyumbani Uwanja wa Manungu kucheza na Mwadui FC ya Shinyanga na Prisons itakuwa nyumbani Uwanja wa Sokoine kuchuana na Ndanda FC ya Mtwara na Coastal Union itakuwa Uwanja wa Mkwakwani ikicheza na Mbeya City.

Maandalizi ya kumwapisha rais mpya yapamba moto

SERIKALI imeendelea kuandaa mazingira ya sehemu itakayotumika kwa ajili ya kumwapisha Rais mteule wa Awamu ya Tano, Dk John Magufuli. Maandalizi ya mazingira hayo yanaenda sambamba na mazoezi ya kijeshi kwa ajili ya gwaride maalumu, litakalofanyika wakati wa kuapishwa kwake katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
HabariLeo lilifanikiwa kutembelea katika uwanja huo na kujionea jinsi mazoezi hayo yanavyoendelea, ambapo mmoja wa askari jeshi aliyekuwa akilinda eneo hilo alisema kinachoendelea ndani ya uwanja huo ni mazoezi ya kijeshi kwa ajili ya siku hiyo.
“Mazoezi ya kijeshi na gwaride yanaendelea humu ndani, kwa sasa wananchi wa kawaida hawaruhusiwi kuingia, ila siku husika ikifika wataruhusiwa,” alisema mwanajeshi huyo. Dk Magufuli anatarajia kuapishwa Novemba 5, mwaka huu baada ya kukamilika kwa taratibu zote za uchaguzi na kukabidhiwa cheti cha ushindi.

CCM haitishwi na wingi wa wagombea

CHAMA Cha Mapinduzi Zanzibar kimesema hakitishwi wala kubabaishwa na wingi wa wagombea wa vyama vya siasa wanaojitokeza kuchukua fomu za urais wa Zanzibar kwani hiyo ndiyo demokrasia ya mfumo wa vyama vingi.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake Kisiwandui mjini hapa, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Vuai Ali Vuai alisema vyama vya siasa vitapimwa kutokana na uwezo wake wa kusimamia na kutekeleza ilani ya uchaguzi iliyojiwekea.
Alisema Chama Cha Mapinduzi kinajivunia na utekelezaji uliotukuka wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010- 2015 ambayo imefanikiwa kwa asilimia 90 katika maeneo yote muhimu ikiwemo ustawi wa jamii, uchumi na sekta ya kilimo.
“ Napenda kuweka bayana kwamba Chama Cha Mapinduzi hakibabaishwi wala kutishika na utitiri wa wagombea wa vyama vya siasa walioibuka katika kinyang'anyiro cha kuchukua fomu kugombea nafasi ya urais wa Zanzibar katika uchaguzi wa Oktoba 25......chama cha siasa kitapimwa na uwezo wake wa kusimamia na kutekeleza ilani ya uchaguzi wake,” alisema.
Katika kinyang'anyiro cha kuwania nafasi ya urais wa Zanzibar tayari jumla ya vyama 15 vimejitokeza kuchukua fomu kuwania nafasi ya urais wa Zanzibar ikiwa hiyo ni mara ya kwanza kuwepo kwa idadi kubwa ya vyama vya siasa.

‘Serikali yalipa madeni yote ya walimu’

SERIKALI imetoa ufafanuzi kuhusu madeni ya walimu kwa kusema imeshalipa yote ya mwaka jana na kwa mwaka huu, orodha inaandaliwa. Orodha kwa ajili ya madeni ya mwaka huu, inasubiriwa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi) kabla ya malipo kufanyika.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk Servacius Likwelile alisema jana kwamba, wakati wa kulipa madeni ya mwaka jana, Wizara ya Fedha ilipokea orodha kutoka Tamisemi ikionesha madeni ya Sh bilioni 19.6. Baada ya kufanya uhakiki, walibaini madeni halali ni Sh bilioni 5.7 ambayo walilipa yote.
Hali inayoonesha kuwa kuna watumishi hewa ambao waliingizwa katika orodha hiyo ya madai. “Sababu za madai hayo kukataliwa ni pamoja na kukosa vielelezo, madai yaliyokwishalipwa, madai yasiyo ya mishahara kuwasilishwa kama mishahara, baadhi ya walimu kutotambuliwa na Halmashauri husika na makosa ya ukokotoaji na uandishi,” alisema Dk Likwelile.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa ufafanuzi huo jijini Dar es Salaam, Likwelile alisema madai ya walimu yako mara mbili ambayo ni mishahara pamoja na madai yasiyo ya mishahara.
Alisema mpaka sasa wizara haijapokea orodha ya madeni ya walimu kwa mwaka huu, hivyo wataanza kuyashughulikia baada ya kuhakikisha walimu wanapata fedha zao kwa wakati. Hata hivyo alisema upo umuhimu wa Tamisemi kuandaa orodha ya madeni na kuyahakiki kutoa orodha ambayo italipwa malipo halali.
Mkaguzi wa Ndani Mkuu, Mohammed Mtonga alisema kutokana na changamoto zilizojitokeza wakati wa uhakiki ikiwemo kuongezwa kwa madai hewa, idara yake inapendekeza kuwa halmashauri zilizowasilisha madai yenye shaka, yasiyo halali au watumishi wasio na madai wawajibishwe kwa kuwasilisha taarifa zisizo sahihi.
Mapendekezo mengine ni kuwa halmashauri hizo zihakikishe zinatenga fedha kwa ajili ya kulipa madai halali ya watumishi wake, kuhakikisha kuwepo kwa rejesta ya madai ya watumishi ambayo hayajalipwa na yaliyolipwa.

Majeshi yamuaga Kikwete

AMIRI Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Rais Jakaya Kikwete amekagua gwaride rasmi lililoandaliwa na vikosi mbalimbali vya jeshi katika sherehe za jeshi hilo ambazo pia zilitumika kumuaga rasmi.
Katika sherehe hizo ambazo zilifanyika katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam jana, walihudhuria wageni mbalimbali. Ndege za kijeshi zipatazo 25 zilipita angani katika uwanja huo kutoa heshima kwa Amiri Jeshi Mkuu huyo ambaye anamaliza muda wa uongozi wake baada ya uchaguzi mkuu, mwezi ujao.
Kikosi cha Makomando wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi (JWTZ) kilionesha uhodari na ujasiri mbele ya Rais Kikwete. Majeshi hayo ya Ulinzi na Usalama ambayo ni pamoja na JWTZ, Jeshi la Magereza, Jeshi la Polisi Jeshi la Wanaanga, Wanamaji walitoa burudani ikiwa ni pamoja na nyimbo kutoka makundi ya sanaa.
Kwenye sherehe hizo za kumuaga Rais Kikwete ambaye hakuzungumza zaidi ya kushuhudia burudani, zilizofanyika sambamba na maadhimisho ya kuzaliwa kwa JWTZ, Septemba Mosi, 1964.

DK. SLAA: SIKUWA LIKIZO, NILIAMUA KUACHANA NA SIASA

Dkt. Slaa akizungumza na wanahabari
-Asema lazima ajitokeze kusema na kuweka ukweli hadharani
-Asema sina tabia ya kuchengachenga nasimamia ninachokiamini
-Mengi yamesemwa na kuandikwa magazetini
-Sina ugomvi na kiongozi yoyote, maana siasa si ugomvi, sina chuki, sina hasira na mtu yeyote
-Siasa inayoongozwa na propaganda, ulaghai ni kuleta vurugu katika taifa na nimekataa hayo
yote.
-Ni kweli nilishiriki katika majadiliano tangu mwanzo
-Misingi niliyoweka ni kwamba Lowassa atangaze kuwa ameachana na chama chake na aeleze anakwenda chama gani kwanza na ajisafishe na tuhuma zake
-Asema hawezi kumsafisha mtu bila yeye kufanya hivyo
-Asema alihoji kama Lowassa anakuja Chadema kama faida au mzigo (assets au liability)
-Asema anataka mgombea mwenye uwezo, sifa na kuiongoza Chadema kuiondoa CCM.
-Kama ni assets anakuja na akina nani? vijana wa mitaani, bodaboda au watu wa aina gani? ni viongozi makini?
-Asema aliambiwa kuwa anahama na wabunge 50, wenyeviti wa mikoa 22, wenyeviti wa CCM wilaya 82.
-Sikupewa majina ya wabunge wala wenyeviti.
-Nikatakiwa kuitisha kikao nikaitisha lakini sikuwa na majibu kama Lowassa ni
Assets au Liability.
-Tangu 2004 sikuwahi kutofautina na mwenyekiti wangu bali tulitofautia kwa hilo.
- Asema aliandika barua ya kujiuzulu kwa M/kiti Prof. Safari barua ikachanwa.
-Siasa ni sayansi haitaki uongo wala ulaghai au propaganda
-Asema mke wake halipwi chochote kutoka Chadema na amekuwa akizunguka nchini kwa mshahara wa Dk. Slaa.
©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved