Profesa Muhongo apinga Tanesco kununua transfoma kampuni binafsi


Waziri wa Nishati ya Madini, Profesa Sospeter Muhongo amepinga uamuzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), kutumia zaidi ya Sh15 milioni kununua transfoma katika kampuni binafsi badala ya kwenye Kiwanda cha Tanalec Limited ambacho shirika hilo lina hisa zake.

Profesa Muhongo alitoa uamuzi huo baada ya kutembelea kiwanda hicho jana akiongozana na maofisa wa Tanesco, Wakala wa Umeme Vijijini (Rea) na maofisa wa wizara hiyo.

Katika ziara hiyo walibaini kuwa Tanesco hainunui transfoma katika kiwanda hicho.

“Kuacha kununua Transfoma Tanalec hakuna sababu nyingine zaidi ya rushwa na siyo kweli kuwa Sheria ya Manunuzi inawabana. Kama kweli inawazuia, suala hili nitalifikisha kwa Rais (John Magufuli) na katika ngazi nyingine za uamuzi,” alisema Profesa Muhongo.

Katika kiwanda hicho, Tanesco inamiliki asilimia 20 ya hisa, Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) asilimia 10 na Kampuni ya Transcentury ya Kenya inamiliki asilimia 70.

Awali, kabla ya ubinafishaji Serikali ilikuwa ikimiliki asilimia 80 za hisa.

Kaimu Meneja Mwandamizi wa Manunuzi wa Tanesco, Jasson Katule alisema shirika hilo linashindwa kununua transfoma Tanalec kutokana na sheria kuwabana kwa kuwa inawalazimisha kutangaza zabuni.

Alisema katika zabuni, Tanalec ilishindwa na kampuni za Quality Group na Intertrade ya India.

Kampuni ya Quality Group itanunua transfoma za zaidi ya Dola 3 milioni za Marekani na Intertrade imeshinda zabuni ya Dola5 milioni za Marekani.

Awali, Meneja Mkuu wa Tanalec, Zahir Saleh alisema kiwanda hicho kwa sasa kina uwezo wa kuzalisha transfoma 10,000, lakini kinazalisha 7,000 kutokana na udogo wake.

Pia, alisema wanakabiliwa na changamoto za kukosa soko la ndani huku wateja wakubwa yakiwa ni mashirika ya umeme ya Kenya, Uganda na Zambia.

Kikwete akubali kuwa balozi wa chanjo Afrika

RAIS mstaafu Jakaya Kikwete amekubali uteuzi wa kuwa Balozi wa Heshima wa kuhamasisha masuala ya afya na kuwataka Wakuu wa Nchi za Afrika kuweka kipaumbele katika upatikanaji wa huduma za afya katika jamii.


Kikwete aliyasema hayo mjini Addis Ababa nchini Ethiopia juzi, wakati akitoa salamu zake baada ya kukubali kuwa Balozi wa Heshima wa ‘Africa United’ kupitia Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na Gavi.

United Africa ni mpango uliobuniwa kusaidia uhamasishaji wa masuala ya afya ukiongozwa na Gavi, CAF, Umoja wa Afrika, Benki ya Dunia na CDC Foundation na wameamua kutumia michezo kama nyenzo mojawapo ya kufanya kampeni ya kuhamasisha jamii juu ya umuhimu wa masuala ya afya yanayolikabili bara la Afrika.

Kikwete, ambaye pia ni Mwenyekiti Mwenza wa Jopo la watu mashuhuri la kumshauri Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa juu ya namna bora ya kuendeleza na kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu hususani katika afya ya uzazi ya mama na mtoto, alisema upatikanaji wa chanjo utasaidia kuokoa vifo vingi vya watoto Afrika.

Uteuzi huo umekuja huku Rais huyo mstaafu akiteuliwa pia kuwa Mjumbe Maalumu wa AU nchini Libya.

Dr. Bana: CCM Iheshimu Mfumo wa vyama Vingi

Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu Cha Dar es salaam ambaye pia ni mchambuzi wa masuala ya kisiasa na mambo ya kijamii Dk Benson Bana amesema chama tawala nchini CCM lazima kikubali utamaduni na kanuni za kukubali mfumo wa vingi vya siasa.


Ameyasema hayo alipokuwa akizungumzia suala la upatikanaji wa Meya wa jiji la Dar es salaam ambapo limegubikwa na mambo ya siasa zizizofaa kwa maendeleo ya wananchi na wapenda demokrasia nchini.

''Kauli za mvutano na malumbano ya UKAWA na chama cha mapinduzi havitasaidia wananchi kwanza wanajidhalilisha, kinachotakiwa ni upinzani kutumia busara lakini chama tawala pia watambue kwamba walipokubali mfumo wa vyama vingi lazima wakubali mabadiliko na kuheshimu mfumo wa vyama vingi

"Hakuna sababu ya msingi ya kuwepo malumbano hadi watu wengine wapigwe na wengine kuwekwa rumande kwanza kazi kubwa ya umeya ni kuongoza vikao ingelikuwa tunatafuta mkurugenzi hapo sawa lakini hili wanakosea kwa kweli''-Amesema Dkt. Bana

Meya wa jiji la Dar es salaam ameshindwa kuchaguliwa mara kadhaa pamoja na kuwepo kwa uhalali wa kufanyika uchaguzi huo jambo ambalo limesababisha malumbano makali na kushikiliwa kwa wabunge wawili wa Chadema Saed Kubenea na Halima Mdee.
==

CHADEMA Kususia ziara na Vikao vya Maendeleo Dar es Salaam


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesusia ziara ya ukaguzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika manispaa za Temeke, Kinondoni na Ilala na kuthibitisha kutoshiriki katika kikao cha bodi ya barabara kinachotarajiwa kufanyika leo kwa kile wanachodai kushinikiza kuachiwa kwa madiwani na mbunge ambao wanaeshikiliwa na jeshi la polisi.

Akielezsea hatua hiyo jana, Meya wa Manispaa ya Kinondoni Boniface Jacob alisema kuwa hawaoni sababu ya kuendelea na vikao mbalimbali vya jiji wakati hawajui hatma ya wenzao ambao mpaka sasa wanashikiliwa na polisi na wengine wanaitwa kufika kituoni hapo kwa kile kinachodaiwa kuwa ni kusababisha fujo katika zoezi la uchaguzi wa meya wa Jiji la Dar es Salaam.

Kikao kikubwa cha kujadili mipango ya maendeleo ya jiji la Dar es Salaam kinatarajiwa kufanyika leo  ambapo mada kuu itakuwa ni ujenzi wa barabara katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Polisi Wafanya Upekuzi Nyumbani Kwa Halima Mdee


Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam jana lilifanya upekuzi mkubwa katika nyumba ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) baada ya kumtilia shaka kuwa na nyaraka muhimu za vikao vya uchaguzi wa Meya wa Jiji hilo.
Kikosi cha jeshi hilo kilifika katika nyumba ya mbunge huyo majira ya saa tisa alasiri na kufanya mazungumzo na Mwanasheria wake, John Mallya ambapo baada ya kukamilisha taratibu za kisheria walianza zoezi la upekuzi uliochukua zaidi ya saa moja.
Kiongozi wa kikosi hicho cha Polisi, aliwaambia waandishi wa habari kuwa walilazimika kufanya upekuzi katika nyumba hiyo baada ya kusadikika kuwa wakati wa vurugu zilizotokea katika ukumbi wa Karimjee jijini humo wikendi iliyopita kufuatia kuahirishwa kwa uchaguzi wa Meya wa Jiji, Mdee aliondoka na faili muhimu lenye madokezo yanayohusu uchaguzi huo.

Hata hivyo, baada ya kukamilisha upekuzi huo, Polisi walijiridhisha kuwa hakukuwa na nyaraka hizo ndani ya nyumba hiyo wala kitu chochote ambacho wangekitilia shaka licha ya kukuta nyaraka nyingi za mbunge huyo. Hivyo, walitoa cheti maalum cha kuthibitisha kuwa hakuwa na nyaraka zozote kinyume cha sheria.
“Wamekagua nyaraka zote. Madai yao ni kuwa Halima alimpora au alichukua nyaraka za kiongozi wa Jiji, lakini wamekuta hakuna jambo lolote ambalo linatiliwa shaka. Na wametoa Certificate inayoonesha kwamba hakuna chochote ambacho kimechukuliwa,” alisema Mwanasheria wa Mbunge huyo, John Mallya.

Mdee alishikiliwa na Polisi na kulala rumande juzi kutokana na tuhuma za kushiriki katika vurugu zilizotokea katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam, Jumamosi, Februari 27.
Wengine wanaoshikiliwa na Jeshi la Polisi ni Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea na Mbunge wa Ukonga, Mwita Waitara.

Wauguzi sita Temeke wasimamishwa Kazi kwa kuuza gloves


Naibu Waziri wa Afya, Dk Hamis Kigwangalla amewasimamishwa kazi wauguzi sita katika hospitali  ya  Temeke kwa kosa la kuomba rushwa.
Wauguzi waliosimamishwa ni Hadija Salum, Beatrice Temba, Agnes Mwampashe, Elizabeth Mwilawa, Mariam Mohamed na Marion Said, ambao walikuwa zamu katika wodi ya wajawazito wakati wa tukio hilo.

“Nimewasimamisha kazi wauguzi wote waliokuwa zamu jana (juzi) asubuhi, nakuagiza Msajili wa Baraza la Wauguzi uwasimamishe hadi utakapowasafisha kupitia kamati ya msajili,” alisema Dk Kigwangalla.
Mmoja wa wajawazito, Loshan Seif alisema alipowasili juzi asubuhi kwa ajili ya kujifungua, muuguzi mmoja wa zamu alimtaka kulipia Sh5,000 za gloves.
“Siku zote huwa natumia bima lakini jana (juzi) wakaniambia hawatumii, nitoe Sh5,000 za gloves, baadaye niliambiwa natakiwa kuwa na uzi wa mshono, sindano na vingine hivyo kama sina nitoe fedha,” Seif.
Dk Kigwangalla alifanya ziara ya ghafla hospitalini hapo jana saa 9.00 alasiri.

Akizungumza jana alasiri baada ya kufanya ziara ya ghafla Hospitalini hapo na kupata malalamiko hayo kutoka kwa wanawake waliojifungua.
“Mama anaambiwa atoe fedha ya gloves Sh5,000 wakati dukani zinauzwa Sh1,000, nataka liwe fundisho kwa wote wanaotuongezea vifo vya wajawazito kwa tamaa ndogondogo,” alisema Kigwangalla.
Katika ziara hiyo, Dk Kigwangalla alishuhudia ubovu wa vyumba viwili vya upasuaji na kutoa maelekezo kwamba, virekebishwe ndani ya miezi sita.
“Hali ni mbaya ndani ya hizi ‘theater’ zote mbili zifanyiwe ukarabati iwapo itashindikana nitazifunga, lazima ziwe na hadhi yake na nitakuja kukagua,” alisema.

Seleiman Jafo Amemvua Madaraka Meneja wa Mamlaka ya Maji Mji Mdogo wa Kisarawe


Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Seleiman Jafo amemvua madaraka Meneja wa Mamlaka ya Maji Mji Mdogo wa Kisarawe mkoani Pwani, Listen Materu kwa kile alichodai ameshindwa kusimamia majukumu yake kikamilifu.
Pia, Jafo ameuagiza uongozi wa halmashauri hiyo kuondoa kero zinazolalamikiwa na wananchi hasa idara za ardhi, afya na elimu.
Akisikiliza kero za wapigakura wake juzi, Jafo alisema uchunguzi alioufanya ameubaini kwa miaka mitano iliyopita kuwa baadhi ya watendaji wa vitengo na idara wa halmashauri hiyo walikuwa hawawajibiki kwa makusudi, lengo lao lilikiwa ni kujenga chuki baina ya mbunge na wananchi jambo ambalo limefikia kikomo.

“Kuna watu waligeuza wilaya hii kama shamba la bibi, walikuwa wanatumia mali za umma kwa kufanya ubadhirifu sasa wasiseme kuwa wamesalimika, kama wamehama au wamehamishwa tutawafuata kokote walipo na watawajibishwa kwa mujibu wa sheria,” alisema.
Naibu waziri huyo alisema, kuwavua madaraka na kuwawajibisha watendaji wabovu hakutaishia kwa watumishi waliopo wilayani hapa, bali hata waliofanya ubadhirifu na kuhama au kuhamishiwa maeneo mengine.
Katika kuboresha wilaya hiyo na kuharakisha maendeleo, Jafo alisema ni wajibu wa halmashauri kuhakikisha inatenga maeneo ya ujenzi wa stendi, machinjio na utekelezaji wake ufanyike haraka na kuwataka iwapo watakabiliwa na changamoto za kukwamishwa mpango huo wasisite kuwasiliana naye.

Mbunge wa Kilombero Peter Lijualikali Akamatwa.

Picha ya maktaba
 
Jeshi la Polisi  Mkoani Morogoro, wilayani Kilombero  jana  lilimkamata mbunge wa jimbo la Kilombero (Chadema), Peter Lijualikali kwa madai ya kutaka kuingia katika kikao cha Baraza la Madiwani cha kuapisha na kuchagua mwenyekiti na makamu wake wakati si mpigakura.

Lijualikali alikamatwa nje ya ukumbi wa halmashauri na polisi na kuswekwa rumande katika Kituo Kikuu cha Polisi Wilaya ya Kilombero saa 3.48 asubuhi wakati akiingia kwenye ukumbi huo kama mmoja wa mashuhuda.

Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Kilombero, Shabaan Mikongolo alisema mbunge huyo hakutendewa haki na polisi kwa kuwa alifika eneo hilo kushuhudia matukio ya kuapishwa kwa madiwani.

“Ni kama kuna maelekezo yalitolewa kwa polisi kuwazuia wabunge, Lijualikali na Devotha Minja (Viti Maalumu – Chadema) na mwakilishi wa Katibu Mkuu Chadema kutoingia ukumbini lakini viongozi wengine wa Serikali ngazi ya mkoa na wilaya waliruhusiwa." Alisema Mikongolo

Pia, polisi walizuia waandishi wa habari na kutaka kuwanyang’anya kamera zao kwa sababu ambazo hazikuwekwa bayana.

Katika uchaguzi huo, Diwani wa Sanje (CCM), David Ligazo alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kilombero kwa kura 19 dhidi ya Godfrey Lwena ( CHADEMA)  aliyepata kura 18

Polisi ,UKAWA Ngoma Nzito........Naibu Katibu Mkuu CUF Nassor Ahmed Mazrui Naye Atakiwa 'Kujisalimisha' Polisi Kwa Mahojiano


Jeshi la Polisi limeendelea na kamatakamata ya wapinzani wa vyama vinavyounda Ukawa katika maeneo mbalimbali likieleza sababu tofauti za kijinai zinazohusishwa na masuala ya kisiasa.

Mpaka sasa wabunge wa upinzani waliokamatwa ni; Halima Mdee (Kawe), Mwita Waitara (Ukonga) na Peter Lijualikali (Kilombero), wote wa Chadema na baadhi ya madiwani wa chama hicho katika Jiji la Dar es Salaam.
Vilevile, imeelezwa kuwa Mbunge wa Ubungo (Chadema), Saed Kubenea alikuwa anatafutwa kuunguanishwa na wenzake.

Pia, baadhi ya wanasiasa wa CUF Zanzibar wamekamatwa na kuhojiwa kwa madai ya kuwatusi viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ). 
Viongozi wa CUF waliohojiwa na polisi mpaka sasa ni Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi, Omar Ali Shehe na Kiongozi wa Mkakati wa Ushindi, Mohamed Sultan Mugheir ‘Eddy Riyami’ ambaye yuko nje kwa dhamana.  

Mbali na viongozi hao, Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui  jana  amepatiwa barua ya wito  na Polisi Zanzibar  ikielezwa kuna mambo yanamhusu.

Hii ni mara ya pili kwa Mazrui kuitwa polisi tangu kufutwa kwa uchaguzi wa Oktoba 25, huku CUF ikidai kuwa huo ni mwendelezo wa mkakati maalumu dhidi ya viongozi wa chama hicho.
Jana, Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa Umma wa CUF, Maalim Hamad Masoud Hamad alidai kuwa hatua hiyo ni utekelezaji wa maagizo ya kisiasa ya kutaka kumkamata kila kiongozi wa juu wa CUF kuelekea uchaguzi wa marudio.

“Kwa viongozi wa CUF hili halishangazi, nahisi ingelikuwa ni hatua ya kushangaza sana iwapo wanaoitwa kuhojiwa na polisi ni viongozi wa vyama vingine.

"Sisi upande wetu hili ni jambo la kawaida mno na watu wasishangae,” alisema.

Mazrui ambaye pia alikuwa Waziri wa Biashara na Uwekezaji, ametakiwa kuripoti Makao Makuu ya Polisi, Ofisi ya Upelelezi Ziwani mjini hapa kesho saa 2.00 asubuhi na kuonana na mkurugenzi wa makosa ya jinai Zanzibar.

Polisi Zanzibar imethibitisha kuwapo wito huo ikisema kuna mambo muhimu yanayomhusu mwanasiasa huyo.

Rufaa ya Babu Seya na Mwanaye Kuanza Kusikilizwa March 11 Mwaka Huu.


Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika (AfCHPR) katika kikao chake kilichoanza jijini Arusha, itapitia maombi ya rufani ya mwanamuziki maarufu nchini, Nguza Viking na John Viking dhidi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hata hivyo, taarifa iliyotolewa na mahakama hiyo jana, ilieleza kuwa kesi hiyo namba 006/2015 iliyopangwa kusikilizwa Machi 11 haitasikilizwa katika mahakama ya wazi.
Ni kesi mbili pekee kati ya 50 zitakazosikilizwa kwenye mahakama ya wazi, ikiwamo inayomhusu mwanasiasa maarufu wa Rwanda, Victoire Ingabire aliyoifungua kupinga ukiukwaji wa haki anaofanyiwa na Serikali yake.

Pia, mahakama ilieleza kuwa kikao hicho cha 40 cha kawaida kitakamilika Machi 18 na kutoa uamuzi wa mashauri manne.
Kesi ya Ingabire inayotarajiwa kuvuta hisia za watu wengi ikizingatiwa upinzani ambao amekuwa akiuonyesha dhidi ya serikali yake, itasikilizwa Machi 4.
Katika kesi hiyo, Ingabire pamoja na mambo mengine anadai haki zake kuvunjwa ambazo zinatajwa kwenye Mkataba wa Mahakama hiyo Ibara ya 7, 10 na 18 hivyo anaitaka itoe uamuzi.

Pia, Taasisi ya Action Pour la Protection des Droits de I’Homme (APDH) inaishtaki Serikali ya Ivory Coast kuvunja mkataba wa Mahakama ya Afrika na Haki za Binadamu Ibara ya 3 na 17 katika kesi namba 001/2014, iliyopangwa kusikilizwa Machi 3.
Mahakama hiyo inaundwa na majaji 11 kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) na inakuwa na vikao vinne kwa mwaka, kufikia Januari 31 tayari ilikuwa imepokea kesi 74 kati ya hizo 25 imetolewa uamuzi.
Maombi manne yamepelekwa  kwa uamuzi zaidi kwenye Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu.

Polisi Yaua Majambazi Watatu....Baada ya Kupekeliwa Walikutwa na Ujumbe wa Kamanda Suleiman Kova


Watu watatu wanaosadikiwa kujihusisha na vitendo vya kigaidi na ujambazi wameuawa katika majibizano ya risasi na polisi.
Watu hao walikutwa na karatasi yenye ujumbe kwa aliyekuwa Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ulioandikwa:

“Nasaha kwa Kova, mzee andaa kamati ya mazishi ya vipolisi vyako tukiwamaliza tutakufikia wewe.”

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alisema jana kuwa tukio hilo, lilitokea Jumamosi iliyopita, eneo la Fire, jijini Arusha wakati mtuhumiwa Athumani Kassim alipokamatwa eneo la Engosheraton akiwa na silaha na aliwataja wenzake.
Kamanda Sabas alisema walipopata taarifa kutoka kwa raia wema walio tilia shaka mwenendo wa mtuhumiwa huyo ambaye alipokamatwa, alikutwa na milipuko, makoti makubwa mawili na kofia ya kuficha uso.
“Baada ya mahojiano, alituambia kuna wenzake wawili anashirikiana nao kufanya uhalifu na tuliweka mtego.

“Saa 5 usiku, askari wetu wakiwa wameambatana na Kassim, walipofika jirani kabisa na nyumba hiyo eneo la Fire, alitoa ishara na wenzake wakaanza kuwashambulia polisi kwa risasi,” alidai kamanda huyo.

Hata hivyo, Sabas alisema polisi waliwazidi nguvu na kuwajeruhi wawili kati yao.
Hata hivyo, magaidi hao walimpiga mwenzao risasi na wao walifariki dunia walipokuwa wakipelekwa hospitali.
Alisema kwenye nyumba waliyokuwa wakiishi, walikuta vitu mbalimbali ikiwamo sare tano za Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kofia tano za kuficha nyuso, vazi moja la karate, pikipiki moja iliyobomolewa na imebandikwa namba bandia.
Alivitaja vitu vingine kuwa ni bendera mbili nyeusi zenye maandishi ya Kiarabu zinazotumiwa na makundi ya kigaidi.

Vitu vingine ni kisanduku cha chuma na hati ya kusafiria ya Abrahaman Athuman Kangaa, iliyotolewa Aprili 2, 2013, simu tano za mkononi na kati ya hizo, moja ilitambulika kuwa ni ya marehemu Mary Joseph aliyefariki kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana Februari 20, mwaka huu, eneo la Engosheratoni pamoja na kifurushi cha unga wa baruti na jambia moja.
Miili ya majambazi hao imehifadhiwa katika hospitali ya Mkoa ya Mount Meru kwa ajili ya utambuzi. 

Makamba Aikosoa Serikali ya Kikwete

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba ametofautisha nyakati za utawala wa Serikali ya Awamu ya Nne iliyoongozwa na Dk. Jakaya Kikwete na zilizopita na huu wa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais John Magufuli, huku akiitoa kasoro iliyopita.
Makamba ameeleza kuwa wakati tawala zilizopita, watu walikuwa wakionewa haya na na kujuana kulichukua nafasi tofauti na awamu hii inayochukua hatua stahiki bila kujali.

“Nadhani moja ya changamoto zilizosababisha huko nyuma tusifanikiwe sana katika suala la uwajibikaji, ni hili suala la kuoneana haya. Suala la kujuana kidogo na kusitiriana,” Makamba aliliambia Gazeti la Mwananchi hivi karibuni.
Alisema kuwa utamaduni huo unapoendelea na kuota mizizi, suala la uwajibikaji huwa kikwazo na hatua stahiki dhidi ya watu wanaofanya makosa hushindwa kuchukuliwa.

Makamba ambaye alikuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia katika Serikali ya Awamu ya Nne, alieleza kuwa hatua za utumbuaji majipu zinazochukuliwa hivi sasa dhidi ya wakwepa kodi na watumishi wanaovunja sheria na kutowajibika ni sahihi na kwamba kama kuna mtu anaona anaonewa bado anayo nafasi ya kutafuta haki yake kwenye vyombo vya kisheria.
“Kikubwa tu ambacho mimi ninaamini ni kwamba kunahitajika kujenga utamaduni mpya wa watu kuogopa na kuheshimu wajibu wao, na kwamba hizi kazi si kazi zetu za kudumu. Wakati wote unapofanya makosa basi kuna Mamlaka ya kukuchukulia hatua,” alisema.

Makamba alisisitiza kuwa ni sahihi kuchukua hatua hivi sasa dhidi ya makosa yaliyofanyika katika utawala uliopita, “Kama huko nyuma hakukuwa na utashi wa mfumo wa kuwezesha makosa hayo kubainika, lakini utashi huo upo sasa, basi hatua zichukuliwe.”

Rais Dkt. Magufuli amtumia salamu za Rambirambi, Rais Mstaafu Dkt. Kikwete kufuatia kifo cha Kaka yake

Mzee Seleman Kikwete enzi za uhai wake

EWURA yatangaza kushuka kwa bei ya mafuta

Mkurugenzi wa Mamlaka ya Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Felix Ngamlagosi amesema ‘kuanzia tarehe 2 Machi bei za mafuta zimebadilika ikilinganishwa na toleo lililopita la Februari 2016.

Kwa Machi 2016 bei ya rejareja za petroli imepungua Tsh 31 kwa lita sawa na 1.70%, Diesel imepungua Tsh 114 kwa lita sawa na 7.10% na mafuta ya taa yamepungua kwa Tsh 234 kwa lita sawa na 13.75%’

‘kwa kiasi kikubwa, kupungua huku kwa bei za mafuta kwenye soko la ndani kumetokana na kuendelea kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia






©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved