Lipumba atangulia urais

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba jana alianzisha mchakato wa kuwania urais kupitia muungano wa kambi ya upinzani nchini unaofahamika kama Ukawa, huku akisema yeye ndiye mtu pekee anayefaa kupeperusha bendera ya vyama vya upinzani.
Akitangaza azma yake ya kuwania urais baada ya kuchukua fomu jijini Dar es Salaam, alisema kutokana na kubobea katika masuala ya uchumi, amefanya tafiti nyingi kuhusu matatizo ya umaskini yanayowakabili wananchi wakati nchi ina rasilimali nyingi; hivyo anajua mahali pa kuanzia mara atakapochaguliwa kuwa Rais wa Awamu ya Tano.
Kama akifanikiwa kutimiza ndoto hiyo, itakuwa historia ya kipekee kwa kambi ya upinzani nchini, kwani tangu uchaguzi mkuu wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi mwaka 1995, CCM ndiyo inayong’ara na hivyo kuendelea kuishika dola.
Aidha, katika chaguzi zilizotangulia tangu 1995, Profesa Lipumba amekuwa akiwania urais mfululizo, lakini kura zake zimekuwa ‘zikipwaya’. Hii ina maana kwamba, anawania urais kwa mara ya tano.
Jana, akizungumza kwa kujiamini, alisema anaamini kuwa rasilimali za taifa hili zikisimamiwa vizuri na kupunguza ufisadi na wizi, fedha za kuiendesha Serikali zipo nyingi na hivyo akasema kuwa iwapo akiteuliwa na Ukawa na kisha kuchaguliwa kuwa Rais hatakuwa na mswalie mtume na mafisadi.
Hata hivyo, Profesa Lipumba alisema yuko tayari kumpigia debe mgombea mwingine wa Ukawa ambaye atasimamishwa na umoja kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi wa taifa, iwapo yeye hatapitishwa.
Umoja huo wa kambi ya upinzani uliokusudia kusimamisha mgombea mmoja wa urais, na pia kuungana mkono kwenye majimbo katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu, unaundwa na CUF, Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved