Mwakyembe, Jaji Ramadhani wagongana Tanga



WAZIRI wa Afrika Mashariki, Dk. Harrison Mwakyembe na Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino Ramadhani, jana walikuwa mkoani Tanga kwa ajili ya kusaka wadhamini ili waweze kukamilisha sharti la kuomba ridhaa ya kugombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza wakati akiwashukuru wanachama wa chama hicho waliojitokeza kumdhamini, Dk Mwakyembe  alizungumzia wingi wa wagombea waliojitokeza kuchukua fomu kwa ajili ya kugombea nafasi ya urais kupitia CCM, akisema umeonyesha ukuaji wa demokrasia.

 “Wenzetu wanatushangaa na wengine wanahoji kwanini nafasi moja inagombewa na watu wengi, lakini niwaambie huku ndio kukua kwa demokrasia ndani ya chama chetu,” alisisitiza Dk. Mwakyembe.

Alisema yeye kwa upande wake anatamani wagombea urais kupitia CCM wafike 50 ili chama kiweze kufanya mchujo ambao utakuwa ni wa haki kwa wanachama wote waliojitokeza katika kinyang’anyiro hicho.

Aidha Mwakyembe alisema ameamua kugombea nafasi hiyo ili kuleta maendeleo, kwani anajua vema changamoto na mafanikio yalipatikana katika serikali ya awamu ya nne.

“Nazijua fursa zilizopo ambazo zitasaidia kutufikisha kwenye mafanikio na maendeleo wakati wa awamu ya tano, hivyo sikuona sababu ya kuingia kinyonge kwenye kinyang’anyiro hicho, kwani mimi ni chaguo sahihi,” alisema.

Kwa upande wake, Jaji Augustino Ramadhani alisema Tanzania si maskini, kwani ina rasilimali nyingi ambazo zikitumika vizuri kwa manufaa ya wananchi zitaleta maendeleo makubwa.

“Ifike mahali wananchi wazinduke pamoja na viongozi rasilimali zilizopo kama madini, utalii, mito na mabonde viwekwe kwenye mfuko wa taifa kwa ajili ya kusaidia watu wote,” alisisitiza.

Aliongeza kuwa nia ya kugombea nafasi hiyo ni kuhakikisha anawatokomeza kabisa maadui watatu, ambao nchi inapambana nao toka enzi ya uhuru, ambao ni umaskini, ujinga na maradhi.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved