Makongoro: Naomba kibali niiokoe CCM dhidi ya rushwa


Butiama. Mtoto wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Charles Makongoro, ametangaza nia ya kuwania urais, akisema anaomba kibali kuisaidia CCM iache rushwa, kuparaganyika na atakapoingia madarakani, ili asiwaangushe Watanzania, anahitaji chama imara kisicho na shaka kama ilivyo sasa.
Akitangaza nia hiyo nyumbani kwao Mwitongo, Butiama jana, Makongoro alisema kutokana na CCM “kubakwa na vibaka,” inawavunja moyo wanachama na inawakatisha tamaa Watanzania, hivyo inahitaji kiongozi anayewarudishia matumaini.
“Sisi ndiyo wazalendo tunasema mnapotaka kutupora hiki chama sisi tupo, turudishieni na mnapoturudishia kipitishie kwa Makongoro Nyerere mna uhakika chama hiki hakipotei siyo kumkabidhi kibaka,” alisema Makongoro.
Kabla ya kutangaza nia hiyo alisema, “nitangaze nisitangaze?, Nitangaze nisitangaze,” akajibiwa na watu waliohudhuria hafla hiyo ‘tangazaaa...’.
Makongoro aliyesema Sh1 milioni za kuchukulia fomu anazo hivyo haitaji kuchangiwa, alikataa kusoma hotuba iliyoandaliwa kwa ajili ya kutaja vipaumbele vyake atakapoingia madarakani na kuwashangaa wenzake waliotangaza nia kwa kutaja vipaumbele, kuwa wanafanya faulo kwa sababu ilani ya chama haijatoka.
Alisema wametangaziwa na chama kuwa ilani itakuwa tayari Julai na kwamba hawezi kutoa kipaumbele vyake halafu baadaye vitofautiane na vitakavyobainishwa na chama ili asije kulaumiwa.
“Nipo hapa kukiri kwamba sehemu kubwa ya tatizo la CCM ni kutofuata utaratibu, ukiona kuna kazi inaombwa kwa kufuata utaratibu na wanaoomba hawafuati utaratibu hawa washtukie mapema, hawafai,” alisema Makongoro na kuongeza:
“Ukiona mtu anayeomba kazi na hafuati utaratibu huo ilhali akiujua, ujue siku ukimpa kazi biashara ya kwanza akifika pale ni kufuta utaratibu huo na kuweka wa kwake ili akae mpaka awe mfalme wa nchi hii, usimpe!”
Makongoro alisema kibaya zaidi viongozi wa CCM ambao wameshiriki kuweka utaratibu huo ndiyo wanahusika na kwamba, ingawa kikao chake hakikuwa cha kuwataja kwa majina walioshiriki kuvunja utaratibu huo lakini hana jinsi lazima awataje.
Aliwataja baadhi ya wagombea waliokwishatangaza nia ndani ya chama hicho akisema wamekiuka utaratibu kwa kutoa ahadi wakati ilani ya chama hao haijapitishwa na mkutano mkuu.
“Wewe (anamtaja mgombea) ni mjumbe wa NEC umeshiriki na unajua kuwa rasimu ya ilani itapitishwa na Mkutano Mkuu wa CCM, wewe unatangulia kimbelembele, nakuuliza wewe nani?”
Makongoro alimpiga kijembe mgombea mwingine akisema hana wasiwasi na uadilifu wala uwezo wa kiongozi huyo lakini hazingatii msamiati wa kung’atuka kwa kuwa amekuwapo ndani ya Serikali kwa muda mrefu.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved