Wagombea waisuta Serikali kwa rushwa

Makada wa CCM waliotangaza nia au kuchukua fomu za kuomba kupitishwa na chama hicho kuwania urais, wameeleza jinsi rushwa, ufisadi na udhaifu katika ukusanyaji kodi huku wakijinadi kuwa wao ndiyo wataondoa uovu huo iwapo watapitishwa kushika nafasi hiyo ya juu kisiasa.
Lakini hakuna hata mmoja aliyeiponda Serikali kwa kushindwa kudhibiti rushwa, ambayo baadhi walishasema kuwa imekithiri hata kwenye chama hicho tawala, huku mmoja akisema kuwa iwapo CCM itampitisha mlarushwa, atajiondoa.
Kati ya waliotangaza nia na kuchukua fomu, makada 11 ni mawaziri wa Serikali ya Awamu ya Nne wakiwamo mawaziri waandamizi walioshika nafasi za juu na waliofanya kazi katika awamu zote nne.
Pia wamo makada waliokuwamo kwenye Baraza la Mawaziri la Serikali ya Awamu ya Nne, lakini wakaondoka kwa sababu tofauti, huku kundi jingine likihusisha watendaji wakuu wa zamani wa Idara ya Usalama wa Taifa.
Lakini bado tatizo hilo la rushwa limekuwa likitumiwa na makada hao wa CCM wanaowania urais wakati wakijinadi kwa wanachama wao kwamba watafumua mfumo uliopo, kusuka upya sheria na kuimarisha taasisi za fedha ili watuhumiwa wakubwa wa rushwa wafikishwe kortini na kufungwa, badala ya kuwakamata walarushwa wadogowadogo pekee.
Katika hotuba zao wakati wanatangaza nia mbele ya umati wa wafuasi wao na mbele ya waandishi wa habari baada ya kuchukua fomu, makada hao, mbali ya kueleza mikakati tofauti ya namna ya kuimarisha uchumi wamekosoa mfumo wa sheria kwamba unawalinda mafisadi wakubwa ambao hawakamatwi hadi kwa kibali maalumu.
Kwa mfano, akitangaza nia ya kuwania urais kijijini kwao Butiama, Charles Makongoro ambaye ni mtoto wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alisema anaomba kibali cha kuisaidia CCM ikomeshe rushwa, na atakapoingia madarakani, ili asiwaangushe Watanzania, anahitaji chama imara kisicho na shaka kama ilivyo sasa.
“Kosa la Rais Jakaya Kikwete ni kuwapenda sana marafiki zake. Kwa bahati mbaya, baadhi ya marafiki zake hao ni vibaka,” alisema Makongoro ambaye ni mbunge wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe aliwaambia wafuasi wake mkoani Lindi kwamba ili kutekeleza utawala bora, hawezi kukaa kimya kuona rushwa, ubadhirifu, ufisadi vikichukua nafasi katika utawala wake.
“Ninawatumia salamu mapema, sitakuwa na kigugumizi kwa wanaotesa Watanzania. Nitahakikisha Watanzania wanachukia rushwa na kutakuwa na sheria kali dhidi ya mtoa na mpokeaji rushwa. Kama ni watumishi wa umma, watakwenda na maji...,” alisema mbunge huyo wa Mtama.
Ahadi ya kukomesha rushwa pia ilitolewa na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta aliyesema kwamba anataka kulifanyia Taifa mambo matano, ikiwa ni pamoja na kutenganisha biashara na siasa na kusimamia maadili ya viongozi wa umma.
“Ili kukomesha tatizo la rushwa, hatuna budi kutunga sheria itakayotenganisha biashara na uongozi,” alisema Sitta kwenye Ikulu ya Wanyanyembe iliyopo Itetemia, Tabora.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved