Kikwete azuia ‘ulaji’ trafiki

  RAIS Jakaya Kikwete ameliagiza Baraza la Taifa la Usalama Barabarani, kuanzisha mara moja mfumo wa ulipaji faini kwa njia ya Benki na mitandao ya simu za mkononi ili kupunguza ushawishi wa vitendo vya rushwa kwa askari wa kikosi cha usalama barabarani nchini.
Pia, ameagiza kuanzishwa mfumo wa kuweka alama kwenye leseni za madereva wanaokiuka sheria na kutumia njia hiyo kuwafungia, ikiwa ni hatua mojawapo ya kudhibiti wimbi la ajali za barabarani hapa nchini.
Rais Kikwete alitoa agizo hilo jana katika viwanja vya Tangamano wakati alipokuwa akizindua Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani Kitaifa, inayofanyika mkoani Tanga, ikiwa imebeba kaulimbiu inayosema ‘Endesha Salama, Okoa Maisha’.
Alisema asilimia 56 ya ajali za barabarani, zinatokana na uzembe na ukosefu wa umakini kwa madereva na kwamba hatua hiyo inasababisha vifo, majeruhi na uharibifu wa mali na hata kuathiri ustawi wa Kaya na Uchumi wa Taifa.
“Hivi mpaka sasa Baraza na Kikosi cha usalama barabarani wanashindwaje kutumia mifumo ya kidigitali kwa nini mpaka leo hakuna kamera barabarani? Kwanza ingesaidia kudhibiti ajali na uvunjaji wa sheria, lakini hata vitendo vya rushwa ambavyo navyo vinachangia ongezeko hili la wimbi wa ajali hapa nchini,” alisema Rais Kikwete.
Alisema katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2010 hadi 2014, jumla ya watu 19,264 walipoteza maisha kutokana na ajali za barabarani na kwamba idadi ya ya waliokufa katika kipindi cha mwaka peke yake ni watu 3,534 sawa na idadi ya wanaopeteza maisha kutokana na ugonjwa wa malaria.
Kufuatia hatua hiyo, amelitaka baraza hilo kufanya mapendekezo ya marekebisho ya sheria za usalama barabarani hasa pale penye mapungufu ili kuweza kusaidia kudhibiti wimbi la ajali linalochangia upotevu wa nguvu kazi ya Taifa.
“Kikosi cha usalama barabarani kiongeze kasi ya kudhibiti ajali za barabarani na kuwachukulia hatua za kisheria Askari wanaojihusisha na vitendo vya rushwa….lakini lisilale katika kutoa elimu ya sheria za usalama barabarani hasa kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari,” alisisitiza Rais Kikwete.
Kwa upande Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani,Naibu Kamishna wa Jeshi la Polisi, Mohamed Mpinga alisema lengo kuu la maadhimisho ya siku hiyo ni kuhamasisha matumizi salama ya barabara pamoja na kuwakumbusha watumiaji namna rahisi ya kutumia barabara ili kupunguza ajali zisizo za lazima.
“Tunapoadhimisha siku hii tunawakumbusha watumiaji kuwa ajenda kuu ya Taifa ni mapambano dhidi ya ajali za barabarani, jambo ambalo linaweza kuadhibitiwa kwa sababu ya uzembe na uvunjaji wa Sheria za Barabarani”,alisema Kamanda Mpinga.
Hata hivyo, alisema katika maadhimisho hayo Baraza limejipanga kufanya Mkutano Mkuu wa wadau utakaoshirikisha nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, sambamba na mafunzo kwa madereva 300 wa daladala na walimu 200 wa shule za msingi kwa lengo la kujenga uelewa kuhusu sheria za usalama barabarani.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga Said Magalula alisema takwimu zinaonesha katika kipindi cha mwezi Januari mpaka Juni mwaka huu, ajali za barabarani zilikuwa 52 ambapo vifo vilikuwa 59 na majeruhi 68. Magalula alisema mkoa huo kwa mwaka 2014 ulifanikiwa kuingia katika tano bora kati ya mikoa ambayo imefanikiwa kudhibiti ajali za barabarani.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved