Mbowe akiri Slaa ‘alimkataa’ Lowassa

MWENYEKITI wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe amekiri kuwa Katibu Mkuu wao, Dk Willibrod Slaa alitofautiana nao katika kumkubali aliyekuwa kada wa CCM, Edward Lowassa kujiunga nao, na sasa amepewa mapumziko.
Dk Slaa amekuwa ‘mafichoni’ tangu Lowassa akubaliwe Umoja wa vyama vinne vya upinzani (Ukawa) kujiunga nao na baadaye kujiunga na Chadema Julai 29, mwaka huu.
Inadaiwa kuwa Katibu Mkuu huyo wa Chadema anapinga kujiunga kwa Lowassa katika chama hicho bila masharti na tangu Waziri Mkuu huyo wa zamani ajiunge nao, ametoweka katika anga za siasa nchini na kumekuwa na maneno mengi kuhusu wapi alipo na kwa nini hajitokezi hadharani katika shughuli mbalimbali za chama hicho.
Lakini akifungua kikao cha Baraza Kuu la Chadema, Dar es Salaam jana ambalo moja ya kazi zake itakuwa kuchambua fomu za Lowassa ambaye ni mgombea pekee wa urais kupitia chama hicho cha upinzani, Mbowe alidai kuwa Dk Slaa ameomba kupumzika na amekubaliwa.
Alikiri kuwa Kamati Kuu ya chama, ilifanya vikao kadhaa kutafakari ujio wa Lowassa na kufanya mashauriano ya muda mrefu na kwamba halikuwa jambo jepesi. Alisema walifanya mashauriano yaliyoambatana na hadhi ya kitafiti ya kisayansi na kuridhika pasipo shaka kuwa ugeni wa Lowassa na wenzake Chadema ni sawa na mpango wa Mwenyezi Mungu uliopaswa kuungwa mkono ili uwasaidie katika azma yao ya kuwaunganisha wenzao wa Ukawa na Watanzania ili kufikia malengo ya pamoja.
“Katika hatua zote hizo tulikuwa sambamba na Mheshimiwa Dk Willibrod Slaa. Katika dakika za mwisho, Dk Slaa akatofautiana kidogo na Kamati Kuu. Tukajaribu kuzungumza naye kwa kina sana, hata jana nimekuwa na kikao na Dk Slaa kwa saa mbili, nimekuwa na kikao naye tena jana mchana,” alisema Mbowe.
Alisema kwa hali ilivyo kwa kuwa uchaguzi uko karibu, maji yakishafika wakati wa kupwa na kujaa, “hayamsubiri “Mbowe, hayamsubiri Slaa, hayamsubiri Baregu, maji yanasonga. Na Mgaya Kingoba

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved