RC acharukia waliofelisha watoto la 7 Tabora

Mkuu wa mkoa wa Tabora mh.Ludovick Mwananzila
MKUU wa Mkoa wa Tabora, Ludovick Mwananzila (pichani), amewaagiza wakurugenzi watendaji wa halmashauri za wilaya kuwaandikia barua za onyo walimu wakuu wote wa shule za msingi waliofaulisha watoto chini ya 10 huku akiwataka pia kuwaondoa mara moja katika madarasa husika walimu waliofaulisha watoto chini ya saba.
Alitoa maagizo hayo jana katika mkutano wa wadau wa elimu uliofanyika Ukumbi wa Mtemi Isike Mwanakiyungi, mjini hapa. Alisema walimu hao wameshindwa kufaulisha kutokana na uzembe na wameshindwa kufanya kazi waliyotumwa na serikali, na kwamba walimu wakuu wameshindwa kuwasimamia wa chini yao ili wafundishe hivyo ambao hawakufundisha ipasavyo na ndio maana yametokea matokeo mabaya ya ufaulu wa darasa la saba 2015.
Aidha, alisema uzembe na vitendo vya ulevi kwa baadhi ya walimu vimechangia pia kufanya vibaya kwa watoto, kwani muda mwingi wanautumia kwenye mambo yao binafsi ikiwemo biashara za bodaboda, ulevi na nyinginezo na sio kufundisha watoto darasani.
Akionesha kuchukizwa na ufaulu duni, Mwananzila aliwaagiza wakurugenzi watendaji wa Halmashauri zote kuwasilisha kwake majina ya walimu walevi na wanaojihusisha na biashara mbalimbali, akisema vitu hivyo vinachangia kurudisha nyuma maendeleo ya elimu. Aliwataka wakuu wa wilaya kusimamia maagizo hayo na kuhakikisha taarifa hizo zinamfikia haraka ili achukue hatua stahiki kwa wahusika.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved