Migiro ajitosa urais, Sitta kurudisha fomu

WAZIRI wa Sheria na Katiba, Dk Asha-Rose Migiro leo anatarajia kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya kuteuliwa kuwania nafasi ya urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Aidha, taarifa zilizozagaa kwenye mitandao ya kijamii, kuwa Waziri wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein kuwa atachukua fomu si za kweli kwa mujibu wa chanzo cha habari kutoka ndani ya CCM.
Migiro, ambaye atachukua fomu kwenye makao makuu wa CCM mjini hapa saa tisa mchana, atakuwa mwanamke wa nne kuchukua fomu za kuwania nafasi hiyo ya juu ya kuiongoza nchi kwa miaka mitano ijayo.
Akiwa ametanguliwa na wanawake wengine Balozi wa Umoja wa Afrika (AU) nchini Marekani, Amina Salum Ally, aliyekuwa Mbunge wa Iringa na pia alishakuwa Naibu Waziri wa Fedha, Monica Mbega, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Dk Mwele Malecela.
Migiro aliyewahi kushika wadhifa wa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), atatanguliwa na kada wa CCM, Salum Marupu ambaye anatarajia kuchukuwa fomu za kuwania nafasi ya urais saa nne asubuhi.
Aidha, katika siku ya leo, Waziri wa Uchukuzi na Mbunge wa Jimbo la Urambo Mashariki, Samuel Sitta anatarajia kurudisha fomu yake baada ya kupata wadhamini katika mikoa 15 ya Bara na Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

©2015 New Day Pro Media.All Rights Reserved